Kuwasaidia Vijana Wakabiliane na Hali Ngumu
ULIMWENGU na mitindo yake
hubadilika daima. Leo, mabadiliko hayo huonekana zaidi kwa sababu ya
teknolojia ya kisasa. Kile kilichokuwa maarufu jana si kitu leo, na
kinachopendwa leo, kesho kitakuwa kimepitwa na wakati. Mabadiliko hayo
ya haraka yamewaathiri sana vijana.
Mabadiliko Makubwa ya Kijamii
Katika miaka ya karibuni,
teknolojia imetokeza mabadiliko makubwa ambayo yamewaathiri sana vijana.
Kwa mfano, katika nchi nyingi vijana huona simu za mkononi na kompyuta
kuwa vyombo muhimu sana vya mawasiliano. Vituo vya kuwasiliana
vimesababisha kuwe na mawasiliano mengi ambayo awali hayangewezekana.
Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 19 nchini Australia anasema hivi:
“Unaweza kuwa huna marafiki wowote, kisha mara moja uwe na marafiki
chungu nzima kwenye Intaneti.”
Watu wengi wanakubali kwamba simu
za mkononi na Intaneti zina manufaa mengi. Hata hivyo, watu wengi huona
kwamba hawawezi kuishi bila vifaa hivyo. Profesa Donald Roberts wa Chuo
Kikuu anasema kwamba wanafunzi fulani “hawawezi kumaliza dakika chache
za mapumziko bila kutumia simu zao za mkononi.” Anasema hivi: “Ni kana
kwamba hawawezi kutulia hadi wazungumze kwenye simu, ni kama wanasema
‘mbona kuna kimya kingi sana.’”
Vijana wengine wanakiri kwamba
hawawezi kuishi bila vifaa hivyo. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 16
aitwaye Stephanie anakiri hivi: “Mimi ni mraibu wa kutuma ujumbe wa
haraka kupitia kompyuta na simu yangu ya mkononi, kwa sababu hiyo ndiyo
njia kuu ya kuwasiliana na marafiki wangu. Ninaporudi nyumbani, mimi
huenda moja kwa moja kwenye kompyuta na kutumia Intaneti mpaka saa tisa
usiku.” Stephanie hulipa kati ya dola 100 hadi 500 kila mwezi kwa ajili
ya gharama za simu. “Kufikia sasa, wazazi wangu wananidai zaidi ya dola
2,000 kwa sababu ya gharama za ziada za simu. Lakini nimezoea sana simu
yangu ya mkononi hivi kwamba siwezi kufanya mambo yangu ya kawaida bila
kuitumia.”
Kuna matatizo mengine zaidi ya
pesa zinazotumika. Alipokuwa anafanya utafiti kuhusu maisha ya familia,
Elinor Ochs, mtaalamu wa tabia na tamaduni za wanadamu aligundua kwamba
mzazi aliporudi nyumbani kutoka kazini, mara nyingi mwenzi wake wa ndoa
na watoto walikuwa wakijishughulisha tu na kile walichokuwa wakifanya
hivi kwamba mara 2 kati ya 3 hata hawakumsalimu! Waliendelea tu kukazia
fikira vifaa vyao vya elektroniki. Ochs anasema, “Tuliona pia jinsi
ilivyo vigumu kwa wazazi kujihusisha katika utendaji wa watoto wao.”
Anaongezea kusema kwamba utafiti huo ulipokuwa ukiendelea, wazazi
walionekana wakijaribu kuepuka kuwasumbua watoto ambao walikuwa
wakikazia fikira mambo waliyokuwa wakifanya.
Je, Kuna Madhara ya Kuwasiliana Kwenye Intaneti?
Wazazi na walimu wengi
wanahangaishwa na muda ambao vijana wanatumia kwenye vituo vya Intaneti
vya kuwasiliana. Vituo hivyo vya Intaneti humwezesha mtu kuanzisha kituo
chake na kukiboresha kwa kuweka picha, video, na habari za kibinafsi.
Jambo linalowavutia watu kutumia
vituo hivyo ni kwamba vinawawezesha kuwasiliana na marafiki. Vilevile
kuanzisha kituo kama hicho humpa kijana nafasi ya kueleza maoni yake.
Inaeleweka ni kwa nini vituo hivyo vinavutia sana vijana kwani kipindi
cha kubalehe ni wakati ambapo kijana hujaribu kujielewa na kueleza hisia
zake katika njia ambayo itawafikia na kuwagusa watu wengine.
Hata hivyo, tatizo moja linalozuka ni kwamba watu fulani hujifafanua kwa kutumia utu wanaotaka kuwa nao badala ya utu wao
halisi. “Kuna kijana katika darasa langu ambaye anasema ana umri wa
miaka 21 na anaishi Las Vegas,” anasema mvulana mmoja mwenye umri wa
miaka 15. Vijana hao wawili wanaishi kilomita 1,600 hivi kutoka Las
Vegas.
Ni jambo la kawaida kwa watu
kutoa habari za uwongo kama hizo. “Unaweza kufanya jambo lolote kwenye
Intaneti,” anasema msichana Mwaustralia mwenye umri wa miaka 18.
“Unaweza kujifanya kuwa mtu tofauti kabisa kwani hakuna mtu anayekujua.
Unajihisi ukiwa na ujasiri. Unaweza kubuni mambo ili uonekane kuwa mtu
mwenye kupendeza zaidi. Unaweza kuingiza picha zako ukiwa umevalia
mavazi ambayo kwa kawaida hungevalia au ukifanya mambo ambayo kwa
kawaida hungefanya. Unaweza kuandika mambo ambayo wewe mwenyewe huwezi
kusema. Unahisi kwamba huwezi kulaumiwa kwa sababu huwezi kupatikana.
Hakuna mtu anayekujua vizuri.”
Kama tu njia nyingine za
mawasiliano, vituo vya Intaneti vya kuwasiliana vinaweza kuwa na manufaa
au madhara. Je, wewe ukiwa mzazi unajua watoto wako wanafanya nini
kwenye Intaneti? Je, unahakikisha kwamba wanatumia wakati wao vizuri?* (Waefeso 5:15, 16) Isitoshe, kutumia Intaneti vibaya kunaweza kumhatarisha kijana kwa njia mbalimbali. Baadhi ya njia hizo ni zipi?
Hatari za Kutumia Intaneti
Kwa kuwa watu wanaotumia
Intaneti hawajitambulishi, watu wanaowavizia watoto ili hatimaye wafanye
nao ngono huona Intaneti kuwa njia rahisi ya kuwanasa. Vijana wanaweza
kunaswa bila kutarajia wanapotoa habari za kibinafsi kwenye Intaneti au
wanapokubali kukutana na mtu ambaye wamekuwa wakiwasiliana naye. Watu
fulani hudai kwamba “watoto hukabili hatari kubwa zaidi ya kufanyiwa
ujeuri au kudhulumiwa ndani ya nyumba zao au mahali wanapochezea,”
kinasema kitabu Parenting 911. “Hata hivyo, jambo
linalowaogopesha wazazi wengi kuhusu watu wanaowavizia watoto ili
wafanye nao ngono ni kwamba wanaweza kuingia nyumbani mwao kupitia
Intaneti na kuwapotosha watoto wao.”
Teknolojia ya mawasiliano
imetumiwa vibaya katika njia nyingine. Vijana wengine wametumia Intaneti
ili kuwaonea wengine, kwa kuwadhihaki, kutoa maoni ya kuwabagua,
kuwasumbua, au kuwatisha. Vituo fulani vimeanzishwa kwa kusudi la
kumwaibisha mtu fulani, ilhali barua-pepe, vituo vya maongezi, na
mitandao kama hiyo imetumiwa kuwachongea wengine. Msimamizi wa kikundi
fulani cha kuangalia usalama kwenye Intaneti anaamini kwamba asilimia 80
hivi ya watoto kati ya umri wa miaka 10 hadi 14, wameathiriwa kwa njia
ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja na uonevu unaofanywa kwenye
Intaneti.
Kwa kweli, uonevu si jambo
jipya. Lakini sasa, uvumi, porojo, na uchongezi zinaweza kusambazwa
mbali na kwa muda mfupi zaidi. Mara nyingi uonevu huo huwa mbaya zaidi.
Katika visa fulani, simu za mkononi zilizo na kamera zimetumiwa kupiga
picha na video zenye kuaibisha, labda mtu akiwa ndani ya chumba cha
kubadili mavazi shuleni au ndani ya bafu. Kisha picha hizo huwekwa
kwenye Intaneti na kutumwa kwa watu wanaotaka kuzitazama.
Jambo Linalozidi Kuhangaisha Jamii
Tatizo hilo lilisababisha Idara
ya Sheria na Usalama wa Umma huko New Jersey, Marekani, kuwatumia wazazi
na walezi barua iliyokuwa na himizo hili: “Tusaidieni kukabiliana na
tatizo linalozuka la matumizi yasiyofaa ya Intaneti miongoni mwa watoto
wakiwa ndani au nje ya shule.” Barua hiyo ilieleza waziwazi hangaiko la
idara hiyo kuhusu kuweka habari za kibinafsi na picha kwenye Intaneti.
Vituo vinavyotoa habari kama hizo huwavutia walaghai wawe vijana au watu
wazima. Barua hiyo ilisema hivi pia, “Wazazi mnapaswa kujua kwamba
mahangaiko haya ni ya kweli na mnaweza kuchangia sana kuwalinda
watoto wenu kwa kujifunza mengi kuhusu Intaneti na kujua vituo ambavyo
watoto wenu hufungua.”
Hata hivyo, wazazi wengine
wanajua machache sana kuhusu yale ambayo watoto wao wanafanya kwenye
Intaneti. Mama mmoja ambaye hufuatilia kwa ukaribu kile ambacho binti
yake mwenye umri wa miaka 16 anafanya kwenye Intaneti anasema hivi:
“Wazazi wanaweza kushtuka na kuaibika sana wakijua mambo ambayo watoto
wao huweka na kuzungumzia kwenye Intaneti.” Kulingana na mtaalamu mmoja
wa usalama kwenye Intaneti, vijana fulani huweka picha walizopigwa
wakiwa wamevalia vibaya.
Madhara
Je, malalamiko hayo yanatoka kwa watu wazima wenye wasiwasi mwingi ambao wamesahau
vituko vyao vya ujanani? Takwimu zinaonyesha hilo si kweli. Fikiria
hili: Katika maeneo fulani, karibu asilimia 33 hivi ya wavulana na
wasichana wenye umri wa miaka kati ya 15 na 17 wamewahi kufanya ngono.
Zaidi ya nusu ya vijana wenye miaka kati ya 13 na 19 wanasema kwamba
wamefanya ngono ya kinywa.
Je, teknolojia imechangia takwimu hizo zenye kushtua? Bila shaka. Ripoti moja katika gazeti New York Times Magazine
inasema kwamba “simu za mkononi na Intaneti, ambazo huwawezesha vijana
kufanya mambo bila kujulikana, hufanya iwe rahisi kwao kukutana na
kufanya ngono bila kuwajibika.” Kwa kweli, inachukua muda mfupi sana
kwenye kompyuta kupanga kukutana kwa siri na mtu wa jinsia nyingine.
Katika uchunguzi mmoja, zaidi ya wasichana 4 kati ya 5 walikiri kwamba
hawawi waangalifu sana wanapotumia Intaneti.
Watu wengine wanaotafuta mchumba
au mtu wa kufanya naye ngono bila kuwajibika wamepata zaidi ya yale
waliyotarajia. ‘Tumeshuhudia ongezeko la visa vya watu kulalwa kwa
nguvu,’ anasema Jennifer Welch wa Idara ya Polisi ya Novato huko
California. Anasema kwamba wahasiriwa wengi huwa wamewasiliana kwanza
kupitia Intaneti na kukubali kukutana na watu ambao baadaye huwadhulumu.
Jihadhari na “Hekima ya Ulimwengu”!
Makala ya kuwashauri vijana
katika magazeti hayachukui msimamo thabiti inapohusu vijana na ngono.
Ingawa wanawatia moyo vijana kuwa safi kiadili au kujiepusha na ngono,
lengo lao kuu ni kuwatia moyo wajihusishe na ngono “salama” badala ya
kutojihusisha hata kidogo na ngono. Ni kama wanasema hivi: ‘Hatuwezi
kuwazuia lakini angalau tunaweza kuwafundisha wawajibike.’
Kwenye makala iliyotolewa kwenye
kituo kimoja cha Intaneti kinachoheshimika ambacho hutoa ushauri kwa
vijana, suala la ama mtu anapaswa au hapaswi kufanya ngono lilitegemea
mambo matatu: (1) hatari za kupata mimba, (2) hatari ya kuambukizwa
magonjwa ya zinaa, na (3) umuhimu wa kuamua kama msichana na mvulana
wako tayari kihisia kufanya jambo hilo. “Lakini wewe ndiye utakayefanya
uamuzi wa mwisho,” kinasema kituo hicho. Kilitaja kijuujuu tu kwamba mtu
anapaswa pia kuzungumzia jambo hilo pamoja na mzazi wake. Makala hiyo
haikutaja kama ni sawa ama si sawa kwa vijana kufanya ngono.
Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka
ungependa watoto wako waongozwe na maoni bora zaidi kuliko “hekima ya
ulimwengu” ambayo ni ya kipumbavu. (1 Wakorintho 1:20)
Unaweza kuwasaidiaje wapite kipindi cha kubalehe na kuepuka hatari
zilizozungumziwa katika makala hii? Jibu haliwezi kuwa tu kufunga
kompyuta au kuwanyang’anya simu. Kusuluhisha mambo kijuujuu hakugusi
mioyo. (Methali 4:23)
Kumbuka pia kwamba huenda watoto wakawa wanatumia vifaa kama simu na
Intaneti kutosheleza mahitaji fulani ambayo ukiwa mzazi unaweza
kuyatosheleza kwa njia bora. Ni nini baadhi ya mahitaji hayo?
[Maelezo ya Chini]
Badala ya wazazi
kushutumu Intaneti, wanapaswa kujua vituo ambavyo watoto wao hupenda
kuvifungua. Kwa njia hiyo, watoto wanaweza kusaidiwa ‘kuzoeza nguvu zao
za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Mazoezi kama hayo kutoka kwa wazazi yatawasaidia watoto wanapokomaa.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
“Ninaporudi nyumbani mimi huenda moja kwa moja kwenye kompyuta na kutumia Intaneti mpaka saa tisa usiku”
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Unaweza kufanya jambo lolote kwenye Intaneti. Unaweza kujifanya kuwa mtu tofauti kabisa kwani hakuna mtu anayekujua”
[Blabu katika ukurasa wa 7]
“Wazazi wanaweza kushtuka na kuaibika sana wakijua mambo ambayo watoto wao huweka na kuzungumzia kwenye Intaneti”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
Vituo vya Kuwasiliana—Simulizi la Msichana Mmoja
“Nilianza kutumia kituo cha
Intaneti cha shule yetu kuwasiliana na wanafunzi wenzangu na walimu.
Nilianza kutumia saa moja kila juma kwenye kituo hicho. Baada ya muda
nikaanza kukitumia kila siku. Nilikuwa nimenaswa sana hivi kwamba wakati
ambapo sikuwa nikitumia Intaneti nilikuwa nikifikiria kuihusu. Sikuweza
kukazia fikira kitu kingine chochote. Sikuweza kumaliza kazi yangu ya
shuleni wala kukaza fikira nilipokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, na
hata niliwapuuza marafiki wangu. Mwishowe, wazazi wangu walitambua
kilichokuwa kikiendelea nao wakaniwekea vizuizi. Ilikuwa vigumu kwangu
kukubali vizuizi hivyo. Nilikasirika sana. Lakini sasa ninafurahi kwamba
wazazi wangu walifanya hivyo nami nimefanya mabadiliko yanayofaa.
Nisingependa kuhisi nimenaswa tena!”
No comments:
Post a Comment